Wednesday, March 12, 2014

Jaji Werema ampa tano Lissu

Dodoma. Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema amempongeza Mnadhimu wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Tundu Lissu, kwa kile alichokiita kuwa ni kuwa na kifua kipana cha kujali masilahi ya Taifa.
Jaji Werema alimwaga sifa hizo jana muda mfupi baada ya kupitishwa kwa Kanuni zitakazoongoza   Bunge Maalumu la Katiba.
Mwanasheria huyo anaungana na wabunge wengine akiwamo Christopher Ole Sendeka wa Simanjiro (CCM), ambaye mwishoni mwa wiki alikaririwa akitaka Lissu apewe nafasi ya Waziri wa Katiba na Sheria kwa sababu ni mahiri katika kusimamia utaifa.
Lissu alikuwa miongoni mwa wajumbe waliopitia na kuzichambua kanuni hizo ambazo kwa sehemu kubwa, zilizua migogoro mikubwa wakati zikijadiliwa kabla ya kupitishwa.
“Tufanye kazi ya kukubaliana na kutunga Katiba yetu, tuache ushabiki wa vyama katika mambo ya msingi kama haya, lakini nawataka wajumbe waangalie mfano wa Tundu Lissu, si kawaida yake kufanya mambo ya hekima kama aliyoyafanya lakini amegeuka na kuwa ngome imara ya maridhiano ya kuzitengeneza Kanuni,” alisema Jaji Werema.
Alisema utaifa na uzalendo ndivyo vilivyomsukuma kufanya kazi hiyo bila ya kuangalia upande mmoja wa chama chake.
Akizungumzia misingi ya Kanuni, aliwataka wajumbe kuvumiliana, kuheshimiana na kupeana nafasi wakati wa kuchangia mijadala.
“Mambo ninayowaomba wajumbe kuyazingatia ni uvumilivu, werevu, kuacha mambo ya vyama, kusoma alama za nyakati na kutokuhamaki wakati wa kuchangia,” alisisitiza.

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...