
Dar es Salaam. Hatimaye watumishi waliokuwa wakitafutwa kujaza 
nafasi 70 za mkaguzi msaidizi wa uhamiaji wamepatikana baada ya usaili 
mzito uliohusisha zaidi ya watu 6,000 kati ya zaidi ya watu 10,000 
walioomba nafasi hizo.
Watumishi hao wapya wanatakiwa kuripoti makao 
makuu ya Idara ya Uhamiaji Julai 29, mwaka huu, ikiwa ni mwezi mmoja 
baada ya kuchujwa kutoka idadi ya watu 6,115 waliofanya usaili kwenye 
Uwanja wa Taifa jijini hapa.
Awali, Idara ya Uhamiaji iliwaita watu 10,800 katika usaili lakini hawakufika wote.
Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Ndani, Isack 
Nantanga baadaye alibainisha kuwa baada ya usaili wa watu 6,115, 
walipatikana 1,681 ambao waliingia katika kinyang’yiro cha kusaka 
watumishi 70 waliotajwa jana.
Majina ya washindi hao yaliwekwa bayana katika 
taarifa ya katibu mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani, Mbarak Abdulwakil 
ambaye amewataka watumishi hao wapya wafike kwa wakati.
Taarifa hiyo iliyotolewa kupitia vyombo vya habari
 jana ilisema; “Ni muhimu kufahamu kuwa uchaguzi wa walioitwa kwenye 
ajira umezingatia vipaumbele vya idara na kutoa nafasi kwa waombaji 
kutoka Zanzibar, ufaulu kuanzia alama ya asilimia 50 na kuendelea pamoja
 na jinsia,” ilisema taarifa hiyo.
Usaili huo wa aina yake umebaki kuwa gumzo huku 
baadhi ya wachambuzi wa masuala ya uchumi na ajira wakitaja kuwa ni 
dalili za wazi kuwa bomu la ukosefu wa ajira linakaribia kulipuka.
Kundi la wasaka ajira hao lilijumuisha vijana wenye umri kati ya miaka 22 na 30.
No comments:
Post a Comment