VIONGOZI
 na Wanachama wapatao 50 wa Klabu ya Simba Jana walitembelea eneo la 
mradi wa uwanja wao ulioko Bunju ‘B’ jijini Dar es Salaam.
Katika ziara hiyo, Wanachama hao 
walifanya kazi ya kulisafisha eneo hilo kwa kufyeka ikiwa ni hatua za 
awali za kutaka kuuendeleza, ambalo linakadiriwa kuwa na eka 25.
Lengo la kufanya ziara pamoja na 
kusafisha eneo hilo ni mkakati wa klabu hiyo, kutaka kuanza rasmi 
mipango ya uendelezaji wa eneo hilo.
Eneo
 hilo linatarajiwa kujengwa uwanja wa mpira utakaokuwa ukimilikiwa na 
klabu hiyo, pamoja na majengo mengine muhimu yatakayoendana na sura ya 
kimichezo.
Katika hatua za awali, klabu hiyo 
imepanga kufyeka pamoja na kupitisha greda lengo likiwa ni kusafisha 
eneo hilo tayari kwa ujezi wa uwanja utakaoweza kutumiwa na timu yake 
kwa ajili ya mazoezi na mechi nyingine za kirafiki.
Katibu Mkuu wa Simba, Ezekiel Kamwaga, 
ameahidi mpaka kufikia Aprili mwaka huu eneo hilo litakuwa na sura ya 
kiwanja cha michezo huku jitihada zingine zikiendelea kufanywa na 
Uongozi kwa ajili ya mradi mkubwa wa kituo hicho ambacho hapo baadaye 
utahusisha hosteli ya wachezaji, mgahawa, gym pamoja na bwawa la 
kuogelea.
Kwa mujibu wa Katibu Mkuu, mpango wa awali utahusisha kuzungusha uzio eneo lote pamoja na ujenzi wa uwanja wa kuchezea mpira.
Kamwaga alisisitiza mradi wa ujenzi 
mkubwa wa eneo hilo bado unafanyiwa kazi na uongozi wa klabu hiyo ili 
kumpata  mkandarasi atakayesimamia ujenzi huo na mipango itakapokuwa 
tayari basi itawekwa wazi isipokuwa kwa sasa wanachofanya ni hatua za 
awali za uendelezaji wa eneo hilo.
Asha Muhaji 
Ofisa Habari 
Simba Sports Club
No comments:
Post a Comment